Halloween Costume ideas 2015

KAZI YA SHETANI -5

JINA LA HADITHI – KAZI YA SHETANI
SEHEMU YA         - TANO
MWANDISHI        - ASLAM KHAN
aslamstorymail@gmail.com
aslamstori.blogspot.com

Iliposhia…

“tusipoangalia hapa, tutashindwa vibaya sana kwa siku zijazo, hilo ni kutokana na kushindwa kupatikana kwa kito chenye rangi ya bluu kilichopo katika kisiwa kimoja katika dunia” alisema mfalme
“nimekuelewa kiogozi wangu mtukufu!”alijibu Edmund.
“je kuna taarifa nyengine ya ziada?” aliulliza mfalme
“ndio kiongozi, kuna Magreth Kimario na Lawrence Majoka walitaka kuja huku ili kukamilisha kafara zao juu ya mahitaji yao kama walivyoahidi, wanasubiria ruhusa yako tu” alisema Eldon.
“Edmund taarifa hizi ni za kweli?” mfalme aliuliza.

Endelea…

“ndio mfalme!”
“sasa wape taarifa kuwa tutakutana katika kikao chetu kitakachofanyika siku zijazo huko huko duniani. Kwa sasa lazima tule sahani moja na maadui zetu wanaojitokeza. Nataka mpaka kesho niwe tayari nimeshapata taarifa zote kuhusu wale wasaliti ambao nimewatambua, wengine lazima muwafuatilie kwa umakini wa hali ya juu sana, hata Kopsha pia simuamini kwa sasa, ila ufuatiliaji wa Kopsha unahitaji akili na ustadi wa hali ya juu, musifanye makosa hata kidogo, mkikosea tu, itatugharimu sisi sote!” alisema mfalme
“sawa mfalme”
“haya, watu wote wa baraza twendeni katika ukumbi wa kifalme, Jackson tutaonana wakati mwengine, nenda ukafanye shughuli nyengine, kikao kimeisha kwa leo”alisema mfalme na kutoka katika kile chumba cha siri na baadhi ya washirika wake ambao walikuwa ni watiifu kwake. Edmund Jackson alitoweka tu ghafla kwa maajabu.
                                                  *******************************************************
Tulibaki vinywa wazi tukistaajabu na kujiuliza maswali mengi kuhusu majibu aliyokuwa ameyatoa Shebby. Kwa nini alijifanya hapajui kumbe anapajua hapa, alikuwa ana nia gani kwetu.tulijiuliza maswali mengi yasiyo na majibu ya uhakika.
“ulishawahi kufika hapa?” yule mzee alimuuliza Shebby. Wote tulikuwa makini kuyasikiliza majibu ya Shebby.
“hapana, sijawahi kufika katika eneo hili hata mara moja katika maisha yangu!” alijibu Shebby.
“ulipajuaje hapa?”
“kwa kusoma vitabu, mimi ni mpenzi mkubwa wa kusoma vitabu na pia kusoma vitabu vya mitandaoni. Kuna siku moja niliwahi kusoma kitabu kilichokuwa kinaelezea uwepo wa nchi ambayo mazingira yake ni tofauti kabisa na mazingira tuliyoyazoea sisi, kwa jinsi mazingira yake yalivyo unaweza kufananisha na mazingira yanayopatikana katika katika bara la Antarctica lenye kutawaliwa na barafu kila upande lakini maajabu ya maeneo haya ni kuwa hakuna baridi kama inayopatikana ndani ya Antarctica. Kwa hali nisiyoitegemea leo nimekuja kuiona mwenyewe” alisema Shebby.
“Bara la Antarctica ndio kitu gani?” aliuliza yule mzee.
“ni moja kati ya sehemu ya nchi kavu kule duniani. Kutokana na hali ya hewa iliyopo, binadamu ni nadra sana kuishi huko. Eneo hilo lipo katika kizio cha kusini cha dunia. Kwa kifupi hakuna makazi ya binadamu yanayopatikana huko!” nilijibu kwa kifupi.
“sawa, vizuri, sasa ngoja niwaambie, yaani mumefanya makosa makubwa sana kufika katika eneo hili. Sio watu nyinyi munaohitajika kuja katika eneo hili. Na mpaka sasa hivi nafikiri kiongozi wa eneo hili tayari atakuwa ameshajua ujio wenu huku, kwa hiyo sijui hata niwasaidieje!” alisema yule mzee.
“mzee wetu, tunaomba utusaidie” alisema Hamza.
“sijui niwasaidie vipi!”
“tafadhali mzee wetu, tungefurahi sana kama ungeweza kutusaidia kupata kurejea nyumbani”
“anhaaa, kwa hilo nitajaribu!”
“samahani mzee naomba kuuliza!” nilisema.
“enhe!”
“mzee kwani hii ni sehemu gani mpaka utuambie sisi hatukupaswa kuja katika eneo hili?”
“wewe ulidhamiria kuja hapa?” alinijibu kwa swali badala ya jibu.
“hapana!”
“unalijua eneo hili?”
“hapana”
“na ndio maana nakuambia haikupaswa nyie kuja katika eneo hili!” alisema kwa msisitizo.
“kwa nini?”
“usiulize maswali mengi, kwani kikubwa ukitakacho ni kitu gani?”
“msaada!”
“sasa subiri kwanza nijaribu kuwapatia msaada mnaouhitaji ila kwa kukusaidia ni kuwa nyie hamkuwa binadamu mnaopaswa kuja huku. Huku huja binadamu maalumu kwa kazi maalumu, kwa mualiko maalumu na kwa wakati maalumu!”
“Binadamu, kazi, mualiko na kazi maalumu?
“ndio, nafikiri umenisikia vizuri!”
“binadamu maalumu ni binadamu wa aina hani hao?”
“binadamu...binadamu sio muda wa maswali na majibu sasa hivi. Mtaniuliza tukifika nyumbani kwangu. Hapa mkikutwa, mtauawa, tuondoke hapa haraka!” alisema yule mzee
“sawa” tulimjibu.”
“chukua hii!” alisema huyu mzee na kutoa fimbo moja yenye rangi nyeupe iliyokuwa inang”aa sana. Pia fimbo ile ilikuwa imenakshiwa kwa kutumia rangi ile ile nyeupe. Ilikuwa na urefu wa sentimita thelathini hivi. Kila mmoja alikuwa anakwepa kuichukua ile fimbo.
“kama mnataka msaada, nimewaambia munisaidie kuibeba hii fimbo, harafu mtanifuata!” alisema yule mzee. aliiacha ile fimbo chini na taratibu akaanza kuondoka. Tulishauriana na wenzangu, kisha niliamua kuichukua ile fimbo na tukamkimbilia yule mzee.
“kitu gani munachokiona?” aliuliza yule mzee mara baada ya kumfikia.
“hakuna kitu tunachokiona zaidi ya jangwa tu!”
“sawa, sasa lazima mpite mule ninamopita mimi, tumeelewana?
“sawa mzee”
“nani aliyeichukua ile fimbo?”
“mimi!” nilijibu.
“masharti ya hiyo fimbo ni kuwa pindi uichukuapo hautakiwi kuiacha kamwe. Na nataka muone faida ya hiyo fimbo, nyoosha kuelekea kule mlikotoka harafu muangalie vizuri”
Nilinyoosha ile fimbo kwa kufuata maelekezo ya yule mzee. Tulikuwa tumeshatembea kwa takribani mita mia tatu hivi. Baada ya kunyoosha, pale tulipokuwa tumesimama kuongea na huyu mzee, tulipata kuwaona viume ambao sikupata kuwafahamu mara moja. Walikuwa wakizunguka zunguka katika eneo lile. Walikaa pale kwa muda kisha wakaondoka kuelekea katika eneo jengin tofauti na upande tuliokuwa tupo sisi.
“mmewaona wale viumbe?” aliuliza yule mzee.
“ndio!”
“munajua pale walikuwa wakifanya nini?”
“hapana!”
“wale ni wapelelezi na wale waliokuwa na rangi nyeusi na kijivu askari kwa ajili ya mauaji. Inavyoonekana taarifa za kuja kwenu hapa zimeshajulikana. Wale wana uwezo wa kujua wanaomtafuta yupo wapi au ameelekea wapi. Pale wameshindwa kujua upande mlioelekea kwa sababu ya hiyo fimbo. Hiyo fimbo ni msaada mkubwa kama itatumika ipasavyo. Hiyo sio fimbo kama munavyoiona. Hiyo ni dagger maalumu yenye uwezo wa kuua mashetani ya kijini na kibinadamu pia. Wote walioshindikana kutokana na uhalifu wao, hapo ndio mwisho wao. Inafanya kazi kutokana na fikra za mtu aliyeichukua. Ina uwezo wa kubadilika na kuwa silaha yeyote kulingana na matumizi ya wakati husika” alisema.
“Dagger ndio nini?” shebby aliuliza 

Je atamjibu kitu gani, usikose sehemu inayofuata.


Labels:

Post a Comment

MKRdezign

Contact Form

Name

Email *

Message *

Powered by Blogger.
Javascript DisablePlease Enable Javascript To See All Widget